Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akiwasilisha hotuba ya ufunguzi rasmi wa Mafunzo elekezi kwa Wahe. Majaji wapya wa Mahakama Kuu.

Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama-Lushoto, Mhe. Jaji Dkt. Gerald Ndika akitoa kwa Wahe. Majaji katika Mafunzo hayo.
Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama-Lushoto, Mhe.Jaji  Dkt. Paul Kihwelo akizungumza wakati wa Mafunzo hayo.

 Jaji Kiongozi, Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Eliezer Mbuki Feleshi akizungumza katika Mafunzo hayo.

Meza Kuu: Katikati ni Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma, wa pili kushoto ni Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama-Lushoto,  ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Gerald Ndika, wa pili kulia ni Jaji Kiongozi, Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Eliezer Mbuki Feleshi, wa kwanza kulia ni Jaji Mstaafu wa Mahakama Kuu, Mhe. Rose Teemba na wa kwanza kushoto ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu-Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Beatrice Mutungi.
Meza kuu katika picha ya pamoja na Wahe. Majaji wapya wanaoshiriki katika Mafunzo elekezi.

 Sehemu ya Wahe. Majaji wapya wakimsikiliza Mhe. Jaji Mkuu alipokuwa akifungua rasmi mafunzo.


Na Magreth Kinabo na Mary Gwera, Mahakama

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amewataka Majaji wapya wa Mahakama Kuu ya Tanzania kuwa sehemu ya maboresho yanayoendelea kufanyika ndani ya Mahakama.

Akifungua rasmi Mafunzo elekezi ya awamu ya tano (5) kwa Wahe. Majaji 12 walioteuliwa na Mhe. Rais hivi karibuni, Mhe. Jaji Mkuu aliwaeleza Majaji hao kuendeleza maboresho ikiwa ni pamoja na kutoa haki kwa wananchi bila kuangalia maeneo waliyopo. 

“Mahakama ya Tanzania kwa sasa ipo katika utekelezaji wa Mpango Mkakati wake wa miaka mitano (5) pamoja na Mradi wa Maboresho ya Huduma za Mahakama (CCP), kwa sasa utekelezaji wake upo katika mwaka wa tatu (3) hivyo nawaalika kuwa sehemu ya muendelezo wa utekelezaji wa maboresho hayo,” alisema Mhe. Jaji Prof. Juma.
Mafunzo hayo yanayofanyika katika Kituo cha Mafunzo na Habari za Kimahakama Kisutu yamefunguliwa rasmi na Mhe. Jaji Mkuu mapema Novemba 18 mwaka huu.
Mbali na hilo, Mhe. Jaji Mkuu aliwataka Majaji hao pia kuzingatia dira na dhima za Mahakama ya Tanzania kwa kuwataka kutoa haki kwa wote na kwa wakati bila upendeleo.

“Mnapotekeleza majukumu yenu msikubali kuingiliwa na mtu yeyote iwe rafiki, mwanafamilia au hata Jaji Mwandamizi juu ya mashauri yaliyopo mbele yenu kwani yapo chini ya mamlaka zenu kikatiba,” alisisitiza Mhe. Jaji Mkuu.

Aliendelea kwa kuwataka Majaji hao kusoma na kuzingatia Kanuni za Mwenendo kwa Maafisa wa Mahakama ‘Code of Conduct for Judicial Officers in Tanzania, 1984’ zitakazowaongoza katika utendaji kazi na vilevile kusimamia na kuviishi viapo vyao.
Awali akimkaribisha Mhe. Jaji Mkuu kufungua rasmi Mafunzo hayo, Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Eliezer Mbuki Feleshi alimshukuru Mhe. Jaji Mkuu kwa kukubali kuruhusu kufanyika kwa mafunzo hayo yatakayoleta tija kwa Majaji hao.

Mhe. Jaji Kiongozi alisema kwa sasa kuna jumla ya Majaji wa Mahakama Kuu 77 ambao kwa wastani kila Jaji anatakiwa kusikiliza jumla ya kesi 518 kwa mwaka  na kuongeza kuwa ingawa idadi hiyo inaonekana ni kubwa jitihada mbalimbali zinaendelea kufanyika zikiwemo za kitaaluma bila kuathiri utoaji wa haki.

“Nina imani kwamba uelewa na uzoefu mkubwa walionao Majaji hawa wapya pamoja na mafunzo wanaoenda kupatiwa yatawawezesha kutoa mchango katika safari ya Mahakama kuelekea Mahakama mtandao ‘e-Judiciary’, kutoa haki kwa viwango vinavyotakiwa na kuwa wawajibikaji wazuri,” alieleza Mhe. Jaji Kiongozi.

Mafunzo ya aina hii yamekuwa yakitolewa kwa Majaji wapya ambapo hupata fursa ya kujengewa uwezo na wabobezi mbalimbali wakiwemo Majaji Wakuu Wastaafu, Majaji wa Rufani na wa Mahakama Kuu waliokwisha staafu.Katika mafunzo hayo kutakuwa na wawezeshaji mbalimbali wakiwemo Majaji waliopo kazini na Wataalamu kutoka Taasisi kadhaa katika sekta ya Sheria na Utumishi wa Umma.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...