Jaji Mkuu wa Tanzania,
Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akiwasilisha hotuba ya ufunguzi rasmi wa Mafunzo
elekezi kwa Wahe. Majaji wapya wa Mahakama Kuu.
Mwenyekiti wa Baraza la
Uongozi wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama-Lushoto, Mhe. Jaji Dkt. Gerald Ndika
akitoa kwa Wahe. Majaji katika Mafunzo hayo.
Mkuu wa Chuo cha
Uongozi wa Mahakama-Lushoto, Mhe.Jaji
Dkt. Paul Kihwelo akizungumza wakati wa Mafunzo hayo.
Jaji Kiongozi, Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Eliezer Mbuki Feleshi akizungumza katika Mafunzo hayo.
Meza Kuu: Katikati ni Jaji Mkuu wa Tanzania,
Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma, wa pili kushoto ni Mwenyekiti wa Baraza la
Uongozi wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama-Lushoto, ambaye pia ni Jaji wa
Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Gerald Ndika, wa pili kulia ni Jaji Kiongozi,
Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Eliezer Mbuki Feleshi, wa kwanza kulia ni
Jaji Mstaafu wa Mahakama Kuu, Mhe. Rose Teemba na wa kwanza kushoto ni Jaji
Mfawidhi wa Mahakama Kuu-Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Beatrice Mutungi.
Meza kuu katika picha
ya pamoja na Wahe. Majaji wapya wanaoshiriki katika Mafunzo elekezi.
Sehemu ya Wahe. Majaji wapya wakimsikiliza Mhe. Jaji Mkuu alipokuwa akifungua rasmi mafunzo.
Na Magreth
Kinabo na Mary Gwera, Mahakama
Jaji
Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amewataka Majaji wapya wa
Mahakama Kuu ya Tanzania kuwa sehemu ya maboresho yanayoendelea kufanyika ndani
ya Mahakama.
Akifungua
rasmi Mafunzo elekezi ya awamu ya tano (5) kwa Wahe. Majaji 12 walioteuliwa na
Mhe. Rais hivi karibuni, Mhe. Jaji Mkuu aliwaeleza Majaji hao kuendeleza
maboresho ikiwa ni pamoja na kutoa haki kwa wananchi bila kuangalia maeneo
waliyopo.
“Mahakama
ya Tanzania kwa sasa ipo katika utekelezaji wa Mpango Mkakati wake wa miaka
mitano (5) pamoja na Mradi wa Maboresho ya Huduma za Mahakama (CCP), kwa sasa
utekelezaji wake upo katika mwaka wa tatu (3) hivyo nawaalika kuwa sehemu ya
muendelezo wa utekelezaji wa maboresho hayo,” alisema Mhe. Jaji Prof. Juma.
Mafunzo
hayo yanayofanyika katika Kituo cha Mafunzo na Habari za Kimahakama Kisutu
yamefunguliwa rasmi na Mhe. Jaji Mkuu mapema Novemba 18 mwaka huu.
Mbali
na hilo, Mhe. Jaji Mkuu aliwataka Majaji hao pia kuzingatia dira na dhima za
Mahakama ya Tanzania kwa kuwataka kutoa haki kwa wote na kwa wakati bila
upendeleo.
“Mnapotekeleza
majukumu yenu msikubali kuingiliwa na mtu yeyote iwe rafiki, mwanafamilia au
hata Jaji Mwandamizi juu ya mashauri yaliyopo mbele yenu kwani yapo chini ya
mamlaka zenu kikatiba,” alisisitiza Mhe. Jaji Mkuu.
Aliendelea
kwa kuwataka Majaji hao kusoma na kuzingatia Kanuni za Mwenendo kwa Maafisa wa
Mahakama ‘Code of Conduct for Judicial Officers in Tanzania, 1984’ zitakazowaongoza
katika utendaji kazi na vilevile kusimamia na
kuviishi viapo vyao.
Awali
akimkaribisha Mhe. Jaji Mkuu kufungua rasmi Mafunzo hayo, Jaji Kiongozi wa
Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Eliezer Mbuki Feleshi alimshukuru Mhe. Jaji
Mkuu kwa kukubali kuruhusu kufanyika kwa mafunzo hayo yatakayoleta tija kwa
Majaji hao.
Mhe.
Jaji Kiongozi alisema kwa sasa kuna jumla ya Majaji wa Mahakama Kuu 77 ambao
kwa wastani kila Jaji anatakiwa kusikiliza jumla ya kesi 518 kwa mwaka na
kuongeza kuwa ingawa idadi hiyo inaonekana ni kubwa jitihada mbalimbali
zinaendelea kufanyika zikiwemo za kitaaluma bila kuathiri utoaji wa haki.
“Nina
imani kwamba uelewa na uzoefu mkubwa walionao Majaji hawa wapya pamoja na
mafunzo wanaoenda kupatiwa yatawawezesha kutoa mchango katika safari ya
Mahakama kuelekea Mahakama mtandao ‘e-Judiciary’, kutoa haki kwa viwango
vinavyotakiwa na kuwa wawajibikaji wazuri,” alieleza Mhe. Jaji Kiongozi.
Mafunzo
ya aina hii yamekuwa yakitolewa kwa Majaji wapya ambapo hupata fursa ya
kujengewa uwezo na wabobezi mbalimbali wakiwemo Majaji Wakuu Wastaafu, Majaji
wa Rufani na wa Mahakama Kuu waliokwisha staafu.Katika
mafunzo hayo kutakuwa na wawezeshaji mbalimbali wakiwemo Majaji waliopo kazini
na Wataalamu kutoka Taasisi kadhaa katika sekta ya Sheria na Utumishi wa Umma.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...