Na Said Mwishehe, Michuzi Globu-Kilimanjaro

SHIRIKA la Kuendelea Kilimohai Tanzania(TOAM) limewahakikishia wakulima ambao wamejikita katika kilimo hicho na hasa katika zao la kahawa kuwa soko la uhakika, hivyo waendelee na jitihada za kuzalisha kwa wingi mazao ya kilimohai nchini.

Limesema linatambua namna ambavyo mazao kama kahawa iliyozalishwa kwa mfumo wa kilimohai ilivyo na soko kubwa na la uhakika duniani na kwamba wanaojihusisha na kahawa hiyo hupata fedha nyingi ukilinganisha na wanaozaisha kwa kutumia sumu na kemikali katika mashamba yao.

Haya yameelezwa leo na Constantine Akitanda, Mshauri wa Mawasiliano wa TOAM mbele ya baadhi ya wakulima wanaofuata mfumo wa kilimohai hai katika kulima zao la kahawa walioko Kata ya Uru Shimbwe mkoani Kilimanjaro baada ya kutembelewa na waandishi wa vyombo mbalimbali vya habari waliokuja mkoani Kilimanjaro kwenye mafunzo maalumu kuhusu kilimohai.

Katika mafunzo hayo ya siku tatu yaliyofadhiriwa na Shirika Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa, (FAO) yanayofanyika mjini Moshi, wanahabari hao watatao 21 kutoka vyombo mbalimbali walipata fursa ya kufanya ziara ya kimafunzo mashambani wakiambatana na maofisa wa TOAM pamoja na FAO huko Shimbwe Juu, kata ya Uru Shimbwe.

Mafunzo kwa Waandishi hao yameandaliwa na TOAM kwa lengo la kuwajengea uwezo katika kuandika kwa umahiri habari za kilimohai.

Akizungumza mbele ya wakulima hao wa kahawa Akitanda amesema kuwa shirika hilo linawahakikishia wakulima kuwa bei ya kahawa iliyozalishwa kwa mfumo wa kilimohai ni bei bora na inayotia matumaini makubwa kwa Wakulima na kwamba mahitaji yake kahawa hai huongezeka kila siku duniani.

"Tunawahakikishia kahawa inayopatikana kupitia mfumo huu wa kilimohai, ina bei inayopendezesha moyo, ndio maana hata hapa kwetu bei ya chini kabisa ni dola za Kimarekani kati ya tano hadi saba ambayo ni wastani wa kuanzia shilingi 10,000/- hadi 15,000 kwa kilo au hata zaidi ya hapo,"amesisitiza Akitanda.

Kwa kukumbusha tu Akitanda aliamua kueleza suala la bei kutokana na kuwepo kwa taarifa ya kwamba bei ya kahawa ya kilimohai kwa wanachama wa AMCOS ya Uru Shimbwe kulalamikiwa vikali na Wakulima hao walipokuwa wakielezea changamoto wanazokumbana nazo katika kuendesha shughuli zao za kilimohai.

Mzee Remmy Temba, mkulima maarufu Shimbwe Juu, aaliwaambia waandishi kuwa kahawa hai kwa sasa wao hulipwa shilingi 4,500 tu kwa kilo moj, napo fedha hizo hulupwa kwa awamu, 2,000awamu ya kwanza na zinazobaki hulipwa awamu ya pili jambo linalowaumiza sana Wakulima wa kilimohai kwa kuwa tofauti ya bei ni ndogo sana baina yao na Wakulima wa kawaida wanaotumia sumu kuulia wadudu na kemikali kukuzia mimea.

Akijibu hoja iliyotolewa na mzee Temba, Akitanda aliwataka Wakulima kuwa na subra wakati jambo hilo likifanyiwa tathimini na uchunguzi.

“Niwaombe sana ndugu zangu wakulima, siku chache zijazo kunafanyika mkutano wa kitaifa kuhusu kilimohai huko Dodoma, kauli mbiu ya mkutano huo ni “Kufikia uhakika na usalama wa chakula, uboreshaji maisha, viwanda na utayari wa kuyakabili mabadiliko ya tabianchi kupitia ubunifu wa kilimohai” aliongeza Akitanda na kusema changamoto hizi zitajadiliwa na kutafutiwa ufumbuzi.

Awali akiwatambushisha Waandishi wa Habari kijijini Shimbwe Juu, Akitanda alisema walifikia uamuzi wa kuwaleta wanahabari Shimbwe kujifunza kwa vitendo kilimohai baada ya kuona jitihada kubwa zinazofanywa na Wakulima wa eneo hilo katika kusimamia misingi ya kilimohai ambayo pia inaheshimu sana kanuni za uhifadhi wa mazingira.

Awali wakulima wa kahawa hai katika mazungumzo yao na waandishi wa habari, waliweka bayana faida za kilimohai na kwamba walisisitiza kuwa hiki ndicho kilimo salama kwa mkulima na mlaji hivyo hawanabudi kukiendeleza na kukirithisha toka kizazi kimoja kwenda kingine.

Wakulima pia walieleza faida anuai za kilimohai pamoja na mambo mengine walisema mazao yake yana thamani kubwa ukilinganisha na mazao yatokanayo na kilimo kisichohai ambacho kwa sehemu kubwa kinategemea mbolea zenye kemikali pamoja na sumu inayotumika kuulia wadudu.

Mzee Remmy Temba amesema kuwa amekuwa akijihusisha na kilimo cha kahawa kwa mfumo wa kilimohai tangu mwaka 1979 kwenye shamba alilorithishwa na marehemu baba yake.

Hata hivyo amesema kuna faida nyingi ambazo anazipata kutokana na kilimo hicho kwa kutoa mifano kadhaa huku akieleza wazi ni kilimo ambacho kimekuwa na tija kubwa kwao ya kijiendesha kiuchumi lakini pia anayekula vyakula vinavyotokana na kilimohai anakuwa ni mtu mwenye nguvu na hatetereki ovyo kiafya kwasababu za magonjwa.

Hata hivyo Diwani wa Kata ya Uru Shimbwe Bertin Mkami amesema kuwa ni kweli changamoto ya wakulima ni bei lakini akatumia nafasi hiyo kueleza sababu zinazosababisha bei kuwa chini. Hivyo Maofisa wa TOAM na FAO walimhakikishia kuwa kilichosemwa kimesikika.
Mkulima wa Kilimohai Lemy Temba wa Kijiji cha Huru Shimbwe akiwa shambani kwake akizungumza na waandishi wa habari hawapo pichani baada ya kutembelea shamba hilo kama sehemu ya kujifunza kuhusu kilimo hicho.Mafunzo yameandaliwa na TOAM
 Mimea ya zao la kahawa ambayo inalimwa kwa mfumo wa kilimohai yakiwa shambani katika Kijiji cha Huru Shimbwe mkoani Kilimanjaro. Shamba  hill ni mali ya mzee Lemy Temba (hayupo pichani)ambaye ameamua kujikita katika kilimo hicho
 Baadhi ya waandishi waliokuwa katika mafunzo ya Kilimohai yaliyoandaliwa na Shirika la Kuendeleza Kilimohai Tanzania( TOAM) wakiwa katika  shamba la Lemy Temba(57) baada ya kwenda kujifunza kuhusu kilimo hicho kwa vitendo. Temba amekuwa akilimiki shamba  hilo tangu mwaka 1979 baada ya kurithi kutoka kwa baba yake.
 Ofisa Mawasiliano wa Shirika la  Kilimo na Chakula la Umoja wa Mataifa( FAO) Emmanuel Kihaule (katikati) akifafanua jambo kwa waandishi wa habari waliohudhuria mafunzo ya kilimohai mkoani Kilimanjaro ambapo waandishi hao walipata nafasi ya kutembelea baadhi ya mashamba yanayolimwa kwa mfumo wa kilimohai yaliyopo Huru Shimbwe mkoani hapa
 Mtalaam  Mshauri wa Kilimohai kutoka Shirika la Kuendeleza Kilimohai Tanzania(TOAM) Costantine Akitanda  akizungumza kuhusu umuhimu wa kilimo hicho na mikakati ya Shirika hilo katika kuhakikisha Watanzania wengi wanaojihusisha nacho kwani kinalipa na kinafaida nyingi za kiafya kupitia mazao yanayotokana na kilimohai kuwa ya asili na yasiyo na kemikali
Baadhi ya waandishi wa habari kutoka vyombo mbalimbali nchini wakiwa katika semina ya kilimohai iliyoandaliwa na TOAM kwa lengo la kuwajengea uwezo wa kuandika habari zinazohusu kilimo hicho na faida zake.Semina hiyo imefanyika jijini Moshi mkoani Kilimanjaro

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...