Na Yassir Simba, Michuzi Tv

ALIYEKUWA Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Kangi Lugola na aliyekuwa Kamishina wa Jeshi la Zima Moto na Uokoaji Thobias Andengenye pamoja na watumishi wengine wa umma 15 wamekutwa  na tuhuma ya makosa, baada ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na rushwa (TAKUKURU) kukamilisha uchunguzi wa makubaliano ya Jeshi la Zima Moto na Uokoaji na kampuni ya ROM solution kupitia mkataba uliohusu upatikanaji wa mkopo wa Euro 408,416,288.16 ambazo ni sawa shilingi Trilioni moja.

Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU Brigedia. Jenerali John Mbungo amesema kuwa uchunguzi huo uliohusu kusainiwa kwa mkataba wa ununuzi wa vifaa vya Jeshi la Zimamoto na Uokoaji wenye thamani ya zaidi ya shilingi trilioni moja kinyume na Sheria za nchi umekamilika kwa asilimia 99.9

Amesema kuwa baada maelekezo ya Rais Magufuli taasisi hiyo ilianza uchunguzi mara moja kwa kukusanya vielelezo na kufanya mahojiano na watu mbalimbali kutoka Wizara ya Mambo ya Ndani, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, watumishi wa Serikali pamoja na makampuni husika.

Amesema kuwa uchunguzi huo uliokamilika kwa asilimia 99.9 ulilenga kuthibitisha iwapo kuna uwezekano wa baadhi ya watumishi kufanya uzembe kwa kutotekeleza majukumu yao ipasavyo na kutozishauri Mamlaka zao kuhusu taratibu mbalimbali za usajili wa makampuni pamoja na uzingatiwaji wa Sheria za ununuzi wa umma.

"Baada ya uchunguzi huu makosa yote tuliyoyagundua yameangukia katika makosa ya uhujumu uchumi ambayo kisheria TAKUKURU haitakuwa na mamlaka ya kuyafikisha mahakamani, kitakachofanyika ni kuwasilisha ni kuwasilisha jalada la uchunguzi katika Ofisini ya Taifa ya Mashtaka ndani ya wiki moja ili kwa kibali chake watuhumiwa waweze kufikishwa mahakamani" Ameeleza Mbungo.

Pia amesema  uchunguzi huo ulilenga kuthibitisha iwapo kuna makosa ya kushawishi, kuomba au kupokea rushwa kinyume na Sheria ya Kuzuia na Kupambana na rushwa namba 11 ya mwaka 2007, pia uchunguzi ulilenga kuthibitisha waliosaini makubaliano hayo kwa niaba ya pande mbili husika kama walikuwa na uhalali wa kufanya hivyo.

"Licha ya hayo uchunguzi huu ulilenga kuthibitisha uhalali wa kisheria wa kuingia makubaliano yoyote ya kizabuni na taasisi za hapa nchini, masuala ya ukwepaji wa kodi halali ya Serikali au ubadhilifu wa mali ya umma pamoja na matumizi mabaya ya madaraka Kama ilivyotamkwa katika Sheria ya Kuzuia na Kupambana na rushwa namba 11 ya mwaka 2007" Ameeleza.

Vilevile amesema kuwa vita dhidi ya ubadhilifu wa fedha, mali pamoja na rushwa ni moja ya kipaumbele Cha Serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Rais. Dkt. John Magufuli ambaye daima amekuwa akisisitiza uwazi na uwajibikaji kwa watumishi na Serikali kwa ujumla.
 Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU Brigedia. Jenerali John Mbungo

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...