Na Karama Kenyunko, Michuzi Globu ya jamii
MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu leo Februari 17 mwaka 2020 imeshindwa kuendelea na makubaliano katika kesi a Uhujumu Uchumi inayomkabili Mwandishi wa Habari Erick Kabendera kwa sababu Hakimu anayesikiliza kesi hiyo amepata udhuru.
Kwa mujibu wa ratiba ya kesi hiyo leo ilitegemewa kuwa ni hatma ya mwisho ya Kabendera kusota rumande tangu alipopandishwa kizimbani Agosti 5,mwaka 2019 baada ya kuingia makubaliano na Mkurugenzi wa Mashitaka nchini (DPP).
Wakili wa Serikali Mwandamizi Wankyo Simon amedai mbele ya Hakimu Mkazi Vicky Mwaikambo kuwa shauri hilo limeitishwa kwa ajili ya kutajwa na Hakimu Mkazi Mkuu, Janet Mtega anayesikiliza kesi hiyo hayupo hivyo ameomba kesi hiyo iahirishwe hadi tarehe nyingine.Hakimu Mwaikambo ameahirisha kesi hiyo hadi Februari 24, 2020 kwa ajili ya kutajwa.
Katika kesi hiyo, Kabendera anakabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi yenye mashtaka matatu likiwemo la utakatishaji wa Sh.Mil 173. Inadaiwa kuwa katika kipindi hicho, Kabendera alijihusisha na mtandao wa kihalifu kwa kutoa msaada kwa genge la uhalifu kwa nia ya kujipatia faida.
Inadaiwa kuwa katika kipindi hicho, bila ya sababu alikwepa kodi ya Sh.Mil 173,247,047.02 ambayo ilitakiwa ilipwe Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA). Pia inadaiwa Kabendera alitakatisha Sh.173,247047.02 huku akijua fedha hizo ni mazalia ya kosa la kujihusisha na genge la uhalifu na ukwepaji kodi.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...