Charles James, Michuzi TV
KATIKA kuendeleza mapambano dhidi ya maambukizi ya ugonjwa wa Corona Mkuu wa Wilaya ya Kongwa, Deo Ndejembi amepokea vifaa vya kujikinga na ugonjwa huo kutoka Taasisi ya Glaring Future Foundation (GFF).
Vifaa hivyo ambavyo ni Ndoo za kunawia na sabuni zake vimekabidhiwa kwa DC Ndejembi na Mkurugenzi wa taasisi hiyo, Aisha Msantu.
Akizungumza baada ya kukabidhiwa vifaa hivyo, DC Ndejembi ameipongeza taasisi ya GFF kwa moyo wao wa uzalendo wa kuiunga mkono serikali dhidi ya vita hii ya Corona kwa kugawa VIFAA hivyo ambavyo vitasaidia wananchi kujikinga na ugonjwa huo.
DC Ndejembi amesema vifaa hivyo vitapelekwa kwenye maeneo yenye mikusanyiko kama vituo vya magari, masoko na kwenye ofisi za serikali ili kila mwananchi anaefika maeneo hayo aweze kunawa mikono kwa maji yanayotiririka na sabuni kama ambavyo wataalam wa afya wanavyosisitiza.
" Huu ni uzalendo mkubwa ambao nyinyi mmeuonesha, hakuna mtu ambaye aliwaomba lakini kwa moyo wenu wa upendo kwetu wanakongwa na watanzania mkaona mtuletee vifaa hivi, tunawashukuru sana.
Niwaahidi kwamba vifaa hivi vitatumika kwenye maeneo yenye mikusanyiko, lakini pia niwaombe msiishie hapa tu tuungane kwa pamoja kwenye sekta nyingine ili tuijenge wote Tanzania," Amesema Ndejembi.
Amewataka wananchi wa Kongwa kuhakikisha wanafuata ushauri wote wa kiafya unaotolewa na serikali katika kipindi hiki ikiwa ni pamoja na uvaaji wa Barakoa, kunawa mikono na kuepuka mikusanyiko isiyo ya lazima.
Amesema ndani ya Wilaya yake wataendelea kutoa elimu ya kujikinga na ugonjwa huo pamoja na kuchukua tahadhari zote ili kuepukana maambukizi ya Corona.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa GFF, Aisha Msantu amesema wataendelea kushirikiana na serikali kwenye mambo mbalimbali ikiwa ni kuunga mkono juhudi zinazofanywa na Rais Magufuli katika kuwaletea maendeleo watanzania.
" Tumeon jitihada zinazofanywa na Rais wetu katika kuwalinda wananchi wake, hivyo tukashawishika kwa kidogo tulichojaliwa basi tuwaunge mkono kwa kulet vifaa hivi hapa Kongwa.
Huu hautokua mwisho ni muendelezo wa ushirikiano wetu kwa serikali ambao tumekua nao kila siku, siyo kwenye afya tu tutaunga mkono kwenye kila jambo ambalo lina maslahi mapana ya watanzania," Amesema Msantu.
Mkuu wa Wilaya ya Kongwa, Deo Ndejembi (wa pili kulia) akipokea msaada wa vifaa vya kujikinga na Corona kutoka katika taasisi ya GFF inayoongozwa na Aisha Msantu (katikati).
Vifaa vya kujikinga na Corona ambavyo vimetolewa na Taasisi ya GFF katika Wilaya ya Kongwa ikiwa ni kuunga mkono juhudi za serikali katika mapambano dhidi ya ugonjwa huo.
Mkuu wa Wilaya ya Kongwa (was tatu kulia) akiwa kwenye picha ya pamoja na viongozi wa Taasisi ya GFF ambao wana tisheti nyekundu baada ya kukabidhiwa vifaa hivyo vya kujikinga na Corona.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...