Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Dkt. Hamisi Kigwangalla ( wa pili kushoto), Katibu Tawala wa mkoa wa Arusha, Richard Kwitega (kulia), Mkurugenzi Mkuu wa NCBA bank Tanzania Ltd, Margaret Karume (wa pili kulia) na kushoto ni Mkurugenzi wa Biashara na Huduma za Kidigitali NBCA bank Gift Shoko, wakionyesha chapa ya Benki mpya ya NCBA Bank Tanzania Limited katika hafla ya uzinduzi wa matawi mapya mawili ya benki hiyo mkoani Arusha

 

 Msanii wa  kike wa Bongo fleva nchini, Nandy akitoa burudani katika hafla ya uzinduzi wa matawi mapya mawili ya benki NCBA Tanzania Limited mkoani Arusha

Benki ya NCBA Tanzania Limited (NCBA) ilifanya uzinduzi wa kihistoria wa matawi yao mawili mapya jijini Arusha jumamosi ya tarehe 19 Septemba. Matawi haya mawili mapya ni Tawi la Clock Tower lililopo Fire Road, Jengo la TFA na Tawi la Sokoine lililopo barabara ya Sokoine, Central Plaza ghorofa ya chini.

 

Hafla hiyo ya uzinduzi ni miongoni mwa matukio yanayoendelea kusherekea ujio wa, Benki ya NCBA, ambayo ni muunganiko wa hiari kati ya NIC (T) Limited na CBA Bank (T) Limited ambapo huduma rasmi za taasisi hii mpya ya Kifedha zilianza Julai 8, 2020 baada ya idhini kutoka Benki Kuu ya Tanzania.

 

Mgeni rasmi wa hafla hio alikuwa Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe Dkt Hamisi Kigwangalla ambaye aliisifu Benki ya NCBA kwa juhudi zao za kuchochea uchumi wa Tanzania. Alisema, ‘Benki ya NCBA imewasili nchini kwa wakati sahihi kabisa, mara tu baada ya Tanzania kujumuishwa kama nchi yenye kipato cha kati huku kukiwa na kiu cha kichocheo kipya kitakachoimarisha nafasi yetu mpya  kiuchumi’.

 

Waziri alielezea kwa kina sehemu muhimu zinazohitaji msaada wa Kifedha mkoani Arusha baada ya athari za ugonjwa wa COVID19. Alinukuliwa, ‘…changamoto zozote zinazoikumba sekta ya utalii zina athari kubwa ambayo moja kwa moja inaathiri sekta nyingine zote za uchumi wa mkoa huu. Hapa Arusha, utalii ukipiga chafya, mji mzima unapata mafua. Na utalii wa Arusha ukipata mafua, basi hali ya utalii nchini kote huambukizwa homa. Hii ni kwa sababu asilimia kubwa ya watalii wanaokuja nchini hutembelea vivutio vya utalii vinavyopatikana katika ukanda huu wa kaskazini.

 

Hata hivyo hivi karibuni tumeanza kuona shughuli za Utalii zikirejea na kuonesha matumaini makubwa ya sekta kuwa kama awali, kurejea kwa shughuli za utalii zitasaidia kuchochea shughuli zingine za kiuchumi. Hivyo nitumie nafasi hii kuhamasisha Banki yenu kusaidia ustawi wa shughuli za Utalii nchini kwa kutoa mikopo ya riba kidogo na kuhairisha ulipaji wa mikopo kwa watoa huduma wa shughuli za Utalii nchini ili kuchochea ukuaji wa sekta hii muhimu kwa uchumi’.

 

Katibu tawala wa Mkoa wa Arusha Mhe Richard Kwitega alimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mhe Idd Hassan Kimanta alikuwa miongoni mwa wageni waalikwa katika hafla hiyo. Aliikaribisha Benki ya NCBA mkoani Arusha na kufafanua maeneo muhimu ya kiuchumi wa mkoa huo. Alisema, ‘Mkoa wa Arusha una fursa kubwa za uwekezaji katika kilimo na biashara husika ambapo mazao ya chakula, kilimo cha bustani na ufugaji kwa ajili ya usalama wa chakula, matumizi ya viwandani na kuuza nje hufanywa. Pia kuna fursa ya kukuza ufanisi katika kilimo cha ufugaji wa samaki’.

 

Alitoa wito kwa Benki ya NCBA kwa kusema, ‘Ni matumaini yangu, Benki ya NCBA imejizatiti kuwainua wakulima katika wigo mzima wa mnyororo wa thamani wa kilimo, kutoka mashambani hadi viwandani. Hii itabadilisha sekta hii muhimu ya uchumi kwa mkoa ili faida zinazopatikana ziifikie jamii na watu binafsi. Bila shaka, hauwezi kuutaja mkoa wa Arusha bila kuzungumzia utalii ambao unachangia zaidi ya 17% kwenye Pato la Taifa’.

 

Vilevile Mkurugenzi Mkuu na Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya NCBA Bi Margaret Karume, aliwashukuru sana wenyeji wa mkoa huo na wageni waheshimiwa kwa kukubali mwaliko wao katika hafla hio na kuikaribisha Benki yao kwa dhati na kuahidi kuwa Benki itakuwa nao bega kwa bega katika safari ya kihistoria na ya pamoja ya mafanikio. Alisema Margaret,

 

‘Benki ya NCBA inaleta kwa pamoja ubora wa dunia mbili. Kuchanganya nguvu za taasisi mbili za awali zinaifanya benki ya NCBA kuwa benki kubwa, na yenye nguvu kifedha, yenye utaalam na uwezo mkubwa unaowaweka wateja wake mstari wa mbele katika kupata mafanikio’. 


Aliendelea kusema, ‘tutafikia malengo yetu kwa kutoa huduma na bidhaa mbali-mbali zita-kazowezesha wateja wetu wa mashirika na wateja binafsi kufanikiwa zaidi kwenye mipango yao. Hii, kwa upande mwingine, itasaidia kufikia matarajio ya ukuaji wa uchumi wa Tanzania. Benki ya NCBA inathamini mahusiano na wateja wetu, na utoaji wa huduma bora kwa kiwango cha kimatiafa ndio kiini cha kila kitu tunachokifanya. Tunaamini kuwa uhusiano mzuri na wa kudumu unajengwa na mafanikio ya kila mmoja’.

 

Benki ya NCBA imezindua matawi 2 mkoani Arusha, yakiwa miongoni mwa matawi 12 mapya nchini baada ya kuzindua Makao ya Makuu ya ofisi na tawi mkoani Dar es Salaam mnamo tarehe 19 Agosti 2020. Benki ya NCBA inatazamia katika siku zijazo kuzindua matawi yake mapya ambayo tayari yameanza kutoa huduma katika mkoa wa Mwanza na visiwani Zanzibar.



Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...