Na Said Mwishehe, Michuzi TV-Kigoma

MGOMBEA Urais kupitia Chama Cha Mapinduzi(CCM) Dk.John Magufuli amesema katika kipindi cha miaka mitano ijayo Serikali yake imepanga kununua meli mbili ambazo zitafanya kazi katika Ziwa Tanganyika.

Miongoni mwa meli hizo mpya, mmoja itakuwa na uwezo wa kubeba mizigo tani 400 na abiria 600 huku meli nyingine itakuwa na uwezo wa kubeba abiria 4000.

Akizungumza leo Septemba 18, 2020, mbele ya maelfu ya wananchi Dk.Magufuli amesema mbali ya kununua meli hizo pia, imepanga kuzifanyia matengenezo meli za MV Liemba ambapo na MV Sangara na kiasi cha Bilioni 16 zitatumika.

"Leo tarehe 18.9 andikeni kuwa tunayosema yanatoka moyoni, mimi sitoi ahadi hewa, nataka Kigoma mfanye biashara , tunanunua meli mpya mbili , nimechoka kusikia ajali kwenye ziwa Tanganyika , hivyo tunataka kutengeneza muelekeo mpya wa Kigoma,"amesema Dk.Magufuli.

Amesema mpango mwingine ni kujenga ofisi kubwa ya bandari ambayo itahudumia bandari zote zilizopo Ziwa Tanganyika, ujenzi wa jengo la abiria na ghala la kuhifadhi mizigo.

Kuhusu usafiri wa anga, Dk.Magufuli amesema ndege zinafaida kubwa na kwamba usafiri kutoka Kigoma hadi Dar es Salaam utakuwa wa urahisi zaidi."

"Tutatanua uwanja wa ndege wa Kigoma ili kurahisisha zitue ndege kubwa, mmenionyesha Zitto Kabwe anashuka kwenye ndege. Nikasema maendeleo hayana chama hata waliopinga ndege wanapanda. Nyinyi Kigoma ni wajanja sana,"amesema Dk.Magufuli.

Amesema usafiri wa ndege ni muhimu, kwani watalii watakuwa wanapitia Kigoma na ili kufanya uchumi kuwa wa kisasa wanataka Kigoma ifaidike na watalii."Tunataka watalii wakija Kigoma waende kwenye mbuga za mbuga Mahale na Gombe na Kigosi."

Dk.Magufuli amesisitiza mipango yote hiyo mizuri ikifanywa na Serikali wanakuja wengine wanasema wameyafanya wao. Kuhusu sekta ya afya katika Mkoa wa Kigoma zimejengwa hospitali tatu za Wilaya ambazo ni wilaya ya Buhigwe, Kasulu na Uvinza, vituo vya afya vipya 10 na kukarabati vingine, 11, dawa na vifaa tiba zimetumika Sh.bilioni 88.27. 98.Pia asilimia 98 ya wanaojifungua wanajifungulia katika vituo vya afya kutoka asilimia 55 kwa mwaka 2015.

Dk.Magufuli amesema changamoto ya kukatika kwa umeme mara kwa mara katika Mkoa wa Kigoma, mkakati wa Serikali imepanga kuunganisha mkoa huo na gridi ya Taifa.



Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...