Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano TANESCO Johari Kachwamba akizungumza wakati wa kikao hicho kinachoendelea Mjini Morogoro.
Meneja Mwandamizi Usambazaji Umeme TANESCO Mhandisi Athanasius Nangali akizungumzia mikakati waliyonayo katika kuhakikisha wanaendelea kuboresha huduma kwa wateja .



Baadhi ya wahariri waandamizi wakifuatilia kwa makini majadiliano yaliyokuwa yakiendelea kwenye kikao kazi kati ya maofisa mbalimbali wa TANESCO na wahariri kutoka vyombo mbalimbali nchini.


Na Said Mwishehe,Michuzi TV-Morogoro

SHIRIKA la UmemeTanzania(TANESCO)limesema katika kuhakikisha wateja wanaendelea kupata huduma bora ya nishati ya umeme wameendelea kufanya maboresha ya miundombinu mara kwa mara huku mkakati uliopo kwa siku za baadae ni kuhakikisha umeme haukatiki kabisa.

Hayo yamesemwa na Meneja Mwandamizi Usambazaji Umeme kutoka TANESCO Mhandisi Athanasius Nangali wakati akizungumza na wahariri wa vyombo vya habari kwenye semina iliyoandaliwa na shirika hilo.

Akifafanua zaidi Mhandisi Nangali amesema "Tunahusika kuhudumia wateja wetu vizuri, kwanza tunasambaza umeme, pili tunaendelea kuwahudumia kipindi chote wanachokuwa wanao umeme ili kuhakikisha wateja wetu wanatapa umeme.

"Tumeendelea kufanya maboresho ya mara kwa mara lengo ikiwa wateja wetu wanapata umeme bora na unaopatikana muda wote ili waendelee na shughuli zao za kimaendeleo.Tunafahamu umeme ni chachu ya maendeleo, umeme ndio unawezesha Tanzania ya viwanda.

"Umeme ndio unaongoza ukuaji wa uchumi, kwa hiyo sisi tujukumu hili tunalo na sasa hivi tunao mpango mkakati wa kukarabati miundombinu yetu ili tufikie malengo ya umeme kutokatika kabisa, ninyi ni mashahidi tulikotoka ni mbali sasa hivi tupo kwenye mafanikio makubwa,"amesema Mhandisi Nangali.

Amesisitiza bado wanataka kufika kwenye hatua ambayo umeme utakuwa haukatiki kabisa."Hii programu tunayo na katika kipindi ambacho tutakuwa tunafanya maboresho, tutakuwa tunatoa taarifa kwa wananchi kupitia matangazao katika vyombo vya habari na mitandao ya kijamii ili wajue nini tunafanya.

Kuhusu wateja wanaohitaji kuunganishiwa umeme, Mhandisi Nangali amewaomba   wafike katika ofisi za TANESCO popote zilipo ili wachukue fomu ambayo inatolewa bure.

"Wasije kupitia kwenye mikono ya vishoka, kwa hiyo wanachi wote waje kuchukua fomu ili waijaze na baada ya kurudisha wawakewe umeme, na sasa hatuna ukiritimba , ukiomba unapewa gharama na ukishalipia unafungiwa  umeme,"amesema Mhandisi Nangali.

Ameongeza na sasa hivi kiwango kikubwa hawacheleweshi katika kuwafungia umeme na wamaendelea kuboresha huduma."Tuko kwenye mpango wa kuhakikisha hapo baadae kidogo mteja anaponunua umeme kwenye simu yake au sehemu yoyote basi umeme unaingia moja kwa moja, hakutakuwa na kuanza kuchukua tokeni na kwenda kuweka katika mita.

"Katika mchakato huo kwa sasa tumeshamuajiri mtaalam mshauri ambaye anapitia maelezo kwa kina na kisha atakapomaliza tutaingia kwenye huo mfumo.Lengo letu sisi mteja awe anapata huduma ya umeme bila matatizo yoyote na kwa urahisi zaidi.

"Mnakumbuka zamani kulikuwa na mita ambazo inabidi usome na kisha uandike bili halafu uirudishe, sasa ni tofauti ila bado tunataka ukinunua umeme basi uende moja kwa moja kwenye mita,"amesema Mhandisi Nangali.

Aidha amezungumzia umuhimu wa wateja wao kufanya ukaguzi kwenye majumba kwani nyumba ikishapata umeme inatakiwe iwe inakaguliwa na mkandarasi aliyethibitishwa na mamlaka za Serikali na ukaguzi huo ni kila baada ya miaka mitano.

"Tumekuwa na kawaida nyumba ikishapata umeme haikaguliwi tena, ni vizuri kufanya ukaguzi kila baada ya miaka mitano na hilo ni jambo muhimu, kwanza litasaidia kuepusha umeme kuvuja,"amesema.

Amefafanua unaweza kuwa unalipia umeme mwingi kumbe unapotelea aridhini.Pia amesema faida nyingine ya kufanya ukaguzi inasaidia kujua iwapo kuna uharibifu, pia inakufanya kama kuna eneo la hitilafu basi ni rahisi mkandarasi kurekebisha kabla ya kuleta madhara.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...