MKURUGENZI Mtendaji wa Bodi
ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB), Abdul-Razaq Badru amesema
taasisi hiyo itaendelea kuzingatia miongozo, sheria, kanuni na taratibu za
utumishi wa umma katika utoaji huduma wa zake kwa wateja.
Akizungumza wakati wa kufunga
mafunzo elekezi ya kuwajengea uwezo watumishi wa HESLB jana (Jumapili Januari,
31 2021), Badru alisema HESLB ni miongoni mwa taasisi za umma zinazogusa
maslahi ya makundi mbalimbali ya kijamii, hivyo inawajibika kuweka mikakati
madhubuti ya kuhudumia wateja.
Badru alisema kwa kutambua
umuhimu huo, Ofisi yake imeandaa miongozo mbalimbali kwa watumishi wake ili
kuwajengea uwezo wa namna bora ya kuwahudumia wateja na kushughulikia
malalamiko yanayojitokeza katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.
“Mafunzo haya ni sehemu
muhimu ya kutukumbusha wajibu wetu katika kuhuhudumia wateja, tukiwa kama
taasisi ya serikali tumeendelea kuboresha utoaji wa huduma kwa wateja kwa
kuzingatia miongozo ya utumishi wa umma ikiwemo kuandaa mkataba wa huduma kwa
wateja na mwongozo wa kushughulikia malalamiko kwa wateja,” alisema Badru.
Aidha Badru alisema kupitia
mada mbalimbali zilizowasilishwa katika mafunzo hayo, ni wakati muafaka kwa
kila mtumishi wa HESLB kutafakari nafasi na wajibu alionao katika kutekeleza
majukumu yake kwa mujibu wa miongozo ikiwemo umuhimu wa kuzingatia uadilifu
sehemu za kazi.
“Tunamaliza mwezi Januari
tukiwa katika mafunzo haya muhimu yanayotukumbusha utekelezaji wa majukumu
yetu, tunapaswa kutimiza wajibu wetu kwa kuzingatia wajibu wa msingi wa kila
mtumishi wa umma na kubwa zaidi ni uadilifu katika maeneo yetu ya kazi”,
alisema Badru.
Awali, Mkurugenzi wa Fedha na
Utawala wa HESLB, Neema Kuwite alisema kutokana na umuhimu wa mafunzo hayo,
Ofisi yake inaandaa mpango wa mafunzo kwa watumishi kuhusu utekelezaji wa
miongozo ya kuhudumia wateja mahali pa kazi kwa kupitia nyaraka mbalimbali
ikiwemo mkataba wa huduma kwa mteja ulioanza kutekelezwa na HESLB.
“Kupitia mafunzo haya
tumepokea ushauri, maoni na mapendekezo kutoka kwa watumishi kuhusu namna ya
kuhudumia wateja wetu, tunaandaa mpango wa mafunzo kwa watumishi ili kuweza
kuwajengea uwezo wa pamoja katika kuhudumia wateja wetu”, alisema Kuwite.
Mafunzo hayo ya siku mbili
yalishirikikisha jumla ya watumishi 140 kutoka Ofisi ya Makao Makuu ya HESLB,
Ofisi za Kanda ya Dodoma, Zanzibar, Mwanza, Mtwara, Arusha na Mbeya.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...