Na Beda Msimbe

TAMTHILIA ya Jua kali  juzi katika Tuzo za kwanza za taifa za filamu ilizoa tuzo nane ikiwamo tuzo ya muigizaji bora wa kike iliyotwaliwa na  Godliver Godian, darekta bora wa kike Leah Mwandamseke, muigizaji bora wa kiume na kike wa kwa chaguo la watazamaji.

Tuzo za chaguo la watazamaji liliwafikia waigizaji watamthilia hiyo ambayo pia ilipata tuzo ya tamthilia bora ni Iddy Kapalata na Maria George. Tuzo nyingine za Jua Kali ni Tuzo za muziki bora wa filamu, Tuzo bora ya mfumo wa uzalishaji na muigizaji msaidizi bora  wa kike iliyokwenda kwa Hellen Herman.

Aidha filamu bora ilienda kwa sinema ya Obambo ambayo pia ilitwaa tuzo ya muigizaji bora iliyokwenda kwa Isarito Mwakalindile, sinematografia bora na  athari maalumu iliyokwenda kwa Ochu na RamarKing na kuwafanya  wawe na tuzo nne.

Aidha katika uitoaji huo wa tuzo Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Innocent Bashungwa  alipokea Tuzo ya Heshima kwa Niaba ya Rais wa Tanzania,Samia Suluhu kwa kutambua mchango wake wa kuiendeleza Tasnia ya Filamu nchini ikiwemo "Royal Tour".

Akizungumza wakati wa utoaji wa tuzo hizo juzi usiku Bashungwa ametoa wito kwa mikoa yote nchini kuiga Mkoa wa Mbeya katika kushirikiana na  Wizara yake  kuandaa Tuzo za Filamu katika miaka ijayo ili kukuza vipaji na kutoa ajira kwa wasanii wengi zaidi walio kwenye mikoa mbalimbali hapa nchini.

Katika tuzo hizo zilizoratibiwa na Bodi ya Filamu chini ya usimamizi wa Wizara ya Utamaduni Sanaa na Michezo, Waziri  Bashungwa
alisema Serikali imeshatenga kiasi cha Sh bilioni 1.5 kwenye mfuko wa Maendeleo ya Sanaa na Utamaduni kwa ajili kukuza na kuendeleza shughuli za Utamaduni na Sanaa ikiwa ni pamoja na Filamu.

“Ninawajulisha kuwa tuzo hizi ni endelevu, hivyo ninawakaribisha wadau wote wenye nia ya kushirikiana na Serikali kwa mwaka 2022.”

Akizungumzia mchakato wa sinema hizo Waziri alisifia sana mchakato ulivyokwenda na kusifia jinsi Tuzo zilivyoweza kuinua vipaji.

Alisema serikali imeanza mwaka huu kwa kutambua nafasi ya tasnia hii kuitambulisha nchi yetu.

Kwa kutambua Mchango wao Mkubwa kwenye Sekta ya Filamu Nchini,Picha za Wasanii Wa Filamu waliotangulia mbele za haki King Majuto,Sharo Milionea,Sajuki na Steven Kanumba ziliwekwa ndani ya Ukumbi wa Tughimbe  zilizokofanyika tuzo.

Akizungumza katika mahojiano baada ya tuzo hizo, Mwenyekiti wa Jopo la Majaji 7 waliohakiki sinema hizo, Profesa Martin Mhando alisema kama majaji  waliipa filamu ya Janga  tuzo kwa kuwa ni filamu inayoonesha mwelekeo chanya wa tasnia.

Alisema sinema hiyo ya Ben Royal  inabidi itazamwe kwa jicho la kipekee kutokana na uhamasishaji wake.

Janga ni filamu iliyoandikwa na John Kokolo ambaye ndiye pia aliyeigiza mhusika Mkuu, ni hadithi inayozungumzia suala la Maji.

"Dhamira hii ni nzito. Ni filamu ambayo kote duniani inaweza kutazamwa kwa hamu  na kuzungumza kwa jinsi inavyolizungumzia Janga la kukosekana kwa maji. Uigizaji wake, mazingira, mandhari na hisia zinazooneshwa zinamkamata mtazamaji kikwelikweli.
Lakini muhimu zaidi ni kuwa filamu inatumia mfumo (genre) ya kusisimua (action) ambayo ndiyo inayouza zaidi duniani lakini sisi Tanzania hatujaweza, au tukiifanya inakuwa kama tunanakili hadithi za wenzetu"alisema Profesa Mhando.

Anasema kwamba jopo imeangalia  na kuona kwamba Janga ni hadithi inayoakisi mazingira ya Kiafrika ingawa ni dunia aliyoibuni mwandishi.

"Tuna matamanio makubwa ya kuona filamu za kibunifu kama hizizikishamiri nchini. " anasema profesa huyo ambaye alisema amefurahi jinsi wasanii walivyopokea matukio hayo.

Akizungumzia tathmini yake kama mtaalamu wa masuala ya filamu alisema filamu nyingi bado zina matatizo ya kutamba na hadithi nyepesi na kusema zile zilizojaribu kumzungumzia masuala mazito zimeonesha upana wa mawazo na uwezo kitaaluma.

"Filamu iliyoshinda kama filamu Bora- inayotwa Obambo ni filamu inayoonesha umahiri kitaaluma kwa kutumia mfumo (genre) ya kitaaluma ya filamu za kutisha. Hapa tumeona ufahamu mkubwa wa dhamira nzito, uwezo wa uigizaji lakini zaidi Dairekta aneonesha ufundi wa hali ya juu ya kutamba na hadithi ya filamu." anasema Profesa Mhando katika mahojiano.

Aidha alisema tamthilia zilizooneshwa zimeonesha ubora katika ufundi (techniques) lakini hadithi zinazotamba ni za kawaida mno kiasi cha kutoweza kuvuka mipaka ya nchi japo ikafika Afrika Mashariki.

"Lazima tutumie ufundi wa waigizaji wetu kutamba hadithi zinazoweza kukamata watazamaji wa kimataifa.  Hilo ni suala la kuangalia na tasnia nzima ikiwa ni pamoja na stesheni za TV kama Azam ambao wakiweza kuwahamasisha kwa kuinua upana wa hadithi na kuwaongezea fedha na muda wa kutengeneza hizo tamthilia. " alisema.

Anasema bila kufanya hivyo tamthilia zetu zitaduma na mwisho wenzetu wa Kenya watakuja kutupiku maana suala kubwa hapa ni tasnia kuifikia hadhira pana ya watazamaji wa tamthilia za Kiswahili.
Wakati huo huo Zaizbar imepanga kumpokea kwa kishindo msanii pekee  aliyeshinda tuzo ya filamu ya Taifa kupitia filamu ya Urithi wa Mila, Mudi Sule.

Wananchi wameombwa leo kuhakikisha kwamba wanakusanyika katika viwanja vya Binti Hamran saa nne kwa ajili ya kumpokea shujaa wao huyo na wasanii wote ambao walikwenda Mbeya kushiriki tuzo hizo.

Ifuatayo ni orodha kamili ya washindi

1. Filamu Fupi  Bora (BEST SHORT FILM)
 MWANDISHI
2. Filamu bora ya kikaragosi (BEST ANIMATION FILM)
 NIVUSHE
3. Filamu Bora ya Dokumentari (BEST DOCUMENTARIES)
 URITHI WA MILA
4. Filamu bora ya Ucheshi (BEST COMEDY)
 SALUNI YA MAMA KIMBO
5. Tamthilia bora ya Ucheshi (COMEDY SERIES (ONLINE/TV)
 KITIM TIM
6. Mcheshi Bora (BEST COMEDIAN)
 MCHUZI JUU (JOTI) - LUCAS LAZARO MHUVILE
7. Tamthilia Bora (BEST SERIES)
 JUA KALI
8. Filamu Bora Ndefu (BEST FEATURE FILM)
 OBAMBO
9. Sinematografia Bora (BEST CINEMATOGRAPHY)
 OBAMBO – FREDDY FERUZI
10. Uhariri Bora (BEST EDITING)
 JANGA - BERNARD EDSON (BEN ROYAL)
11. Mfumo bora wa sauti (BEST SOUND DESIGN)
 MGENI – VINONDO RECORDS
12. Muziki bora wa Sinema (BEST MUSIC SCORE)
 JUA KALI – SELEMANI MASENGA & SWITCH MUSIC GROUP
13. Ubunifu Bora wa maleba (BEST COSTUME DESIGN)
 JANGA – BERNARD EDSON (BEN ROYAL)
14. Mfumo bora wa Uzalishaji (BEST PRODUTION DESIGN)
 JUA KALI – FLORANCE G. MKINGA
15. Muonekano Bora wa Eeneo (BEST SET DESIGN)
 NYARA – ELIUD DOMINIC & KIFUA COMPOUND
16. Ubunifu bora wa Grafiki (BEST GRAPHICS DESIGN)
 NYARA – ELIAS KINOGO (Destro)
17. Athari bora maalumu  (BEST SPECIAL EFFECTS MAKEUP)
 OBAMBO – OCHU KIOTA & RAMAR KING
18. Uchezaji skrini Bora (BEST SCREEN PLAY)
 JANGA - BERNARD EDSON (BEN ROYAL)
19. Darekta bora wa Kike (BEST FEMALE DIRECTOR)
 JUA KALI - LEAH MWENDAMSEKE
20. Darekta Bora wa Kiume (BEST MALE DIRECTOR)
 JANGA – BEN ROYAL
21. Muigizaji Bora wa Kiume (BEST ACTOR)
 OBAMBO – ISARITO MWAKALINDILIE
22. Muigizaji bora wa Kike (BEST ACTRESS)
 JUA KALI – GODLIVER GODIAN
23. Muigizaji Bora Msaidizi wa Kike (BEST SUPPORTING ACTRESS)
 JUA KALI – HELLEN HERMAN
24. Muigizaji Bora Msaidizi wa Kiume (BEST SUPPORTING ACTOR)
 HAIKUFUMA – HUSSEN LUGENDO
25. Muigizaji Bora anayechipukia wa kike (BEST UPCOMING ACTRESS)
 BANTU – BRENDA MALEMBEKA
26. Muigizaji Bora anayechipukia wa kiume (BEST UPCOMING ACTOR)
 HAIKUFUMA – SADAM NAWANDA
27. Muigizaji Bora wa Kiume chaguo la watazamaji (BEST ACTOR AUDIENCE CHOICE)
 JUA KALI – (IDDY KAPALATA) MOHAMEDY KINGARA
28. Muigizaji Bora wa Kike chaguo la Watanzamaji (BEST ACTRESS AUDIENCE CHOICE)
 JUA KALI – (MARIA GEORGE) MARIANNE MDEE




Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...