Chama
Cha Mapinduzi (CCM) kinampongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kuridhia ongezeko la
mishahara na kupandishwa kwa malipo ya mkupuo ya pensheni kwa wastaafu.
Uamuzi
huo wa kupandisha mishahara, ikiwa ni pamoja na kima cha chini kwa
watumishi wa umma kwa asilimia 23.3, ambao umefanyika kwa kuzingatia
taratibu za mwenendo wa uchumi, pia ule wa kuelekeza kukamlishwa kwa
taratibu za kisheria kuhakikisha malipo ya mkupuo ya wastaafu
yanapandishwa kutoka asilimia 25 hadi asilimia 33.
Huu
ni mwendelezo wa hatua kadhaa zinazoendelea kuchukuliwa na Serikali ya
CCM awamu ya sita chini ya uongozi wa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu
Hassan kwa lengo la kuboresha maslahi na stahiki za wafanyakazi nchini.
Tayari serikali ilishapunguza kodi ya mapato katika mishahara ya
wafanyakazi (PAYE) kutoka asilimia 9 hadi 8, kufuta tozo ya kulinda
thamani ya mkopo ya asilimia 6 (Value Retention Fee) kwa wanufaika wa
mikopo elimu ya juu wakati wa marejesho na upandishwaji wa madaraja kwa
kuzingatia miundo ya utumishi wa kada mbalimbali.
Hatua
zote hizi ni sehemu ya utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka
2020 -2025, ibara ya 130, ukurasa wa 180-181. Aidha nyongeza ya
mishahara ni utekelezaji wa ahadi ambayo
Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan aliitoa kwa wafanyakazi kupitia
hotuba yake kwa taifa Siku ya Wafanyakazi Duniani (Mei Mosi, 2022), kuwa
'Jambo lao lipo na linafanyiwa kazi'
Utekelezaji
wake umedhihirisha jinsi Rais Samia Suluhu Hassan alivyo kiongozi
msikivu, anayejali wananchi wake, muungwana wa vitendo na zaidi yuko
imara kuhakikisha Serikali ya CCM anayoiongoza, inaendelea kuwa tumaini
la watu kwa kugusa maisha yao kwa namna chanya.
Vile
vile uamuzi wa nyongeza ya mishahara na malipo ya mafao kwa mkupuo
umefikiwa baada ya kuwepo majadiliano yaliyohusisha serikali na wadau
wanaohusika vikiwemo vyama vya wafanyakazi kupitia Shirikisho la Vyama
vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA) na Chama cha Waajiri Tanzania (ATE).
Mchakato huu umeendelea kuthibitishia dunia kwamba uongozi wa Rais Samia
Suluhu Hassan ni shirikishi na wenye uwazi sifa ambazo ndio msingi wa
utawala bora.
Chama
Cha Mapinduzi kinatoa wito kwa wafanyakazi nchini kuendelea kuiunga
mkono serikali, kushikamana, kufanya kazi kwa bidii, uzalendo na weledi
ili kuleta tija zaidi katika maendeleo ya Nchi yetu.
KIDUMU CHAMA CHA MAPINDUZI.
Shaka Hamdu Shaka,
Katibu wa Halmashauri Kuu Taifa,
Itikadi na Uenezi.
15 Mei, 2022.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...