Daraja la mto Lumbegea linalounganisha kijiji cha Miembenina kijiji cha Likuyumandela lililojengwa na Tarura wilaya ya Namtumbo likiwa limekamilika na kuanza kutumika.Mhandisi wa wakala wa barabara za mijini na vijijini(Tarura)wilayani Namtumbo Samwel Makongwa kushoto na mfanyakazi wa Tarura Hassan Nyoni wakiwaongoza baadhi ya wananchi wa kijiji cha Likuyumandela kuangalia daraja la Mto Lumbegea.
Na Muhidin Amri, Namtumbo
WAKALA wa barabara za vijijini na mijini(Tarura) wilaya ya Namtumbo
mkoani Ruvuma,umeishukuru Serikali ya awamu ya sita kwa kuipatia jumla
ya Sh.milioni 495,000,000 kwa mwaka wa fedha 2020/2021 zilizotumika
kujenga na kuboresha miundombinu ya barabara wilayani humo.
Pongezi hizo zimetolewa jana na Meneja wa Tarura wilaya ya Namtumbo
Mhandisi Fabian Lugalaba, wakati akizungumza kuhusiana na barabara mpya
zilizojengwa na Tarura ambazo zimewezesha kuunganisha vijiji
mbalimbali na kuchochea uchumi wa wananchi.
Lugalaba alisema, kati ya fedha hizo Sh.milioni 90,000,000 zimetumika
kwa ajili ya kujenga(kutoboa) barabara mpya na kiasi cha Sh.milioni
405,000,000 zimetumika kujenga madaraja yaliyowezesha kurudisha
mawasiliano kwa vijiji vya Mgombasi,Miembeni na Likuyumandela.
Kwa mujibu wake,katikati ya kata ya Mgombasi na Likuyuseka kuna kijiji
cha Miembeni ambacho hakikuwa na mawasiliano ya barabara,hivyo
kusababisha wakazi wake kuwa na mazingira magumu pindi wanapohitaji
kwenda maeneo mengine kwa ajili ya kupata huduma ikiwamo ya afya.
Alisema,kutokana na changamoto hiyo serikali iliona umuhimu wa kupeleka
barabara katika maeneo hayo ambapo katika bajeti ya mwaka wa fedha
2020/2021 ilitenga jumla ya Sh.milioni 90 kwa ajili ya
kutoboa(kujenga)barabara mpya itakayounganisha kata hizo na kijiji
hicho.
Lugalala alitaja barabara hizo ni Mfuate-Miembeni-Mgombasi yenye urefu
wa km 17.2 iliyogharimu juma ya Sh.milioni 50 na barabara ya
Likuyumandela-Miembeni yenye urefu km 11.5 iliyojengwa kwa gharama ya
Sh.milioni 40.
Aidha alisema,katika maeneo hayo yote mawili kuna mito ambayo ilihitaji
kujengwa madaraja,ambapo katika barabara ya Mfuate-Miembeni- Mgombasi
kulihitaji daraja la mita 20 katika mto Luegu na limejengwa kwa gharama
ya Sh.milioni 350.
Lugalaba alitaja daraja lingine ni la mita 8 linalounganisha kijiji
cha Miembeni kwenda Likuyumandela ambalo hadi kukamilika limegharimu
sh.milioni 40.
Alieleza kuwa,kwa kutumia fedha zinazoletwa na Serikali zikiwamo za
ongezeko la tozo zilizoasisiwa na Rais Samia Suluhu Hassan,
watahakikisha wanajenga miradi ya barabara kwa ubora wa hali ya
juu,uaminifu,uadilifu na inayoendana na thamani halisi ya fedha
zinazotolewa ili wananchi wengi hasa waishio maeneo ya vijijini wafikiwe
na mtandao wa barabara.
Alisema,malengo ya Tarura ni kuhakikisha maeneo yote ambayo hayafikiki
kwa urahisi wanatumia fedha zinazotengwa na Serikali kufikisha huduma ya
mawasiliano ya barabara ili kuwarahisishia wananchi kufanya shughuli
zao za maendeleo.
Amewaomba wananchi ambao barabara na madaraja yamejengwa,kuhakikisha
wanatunza miundombinu hiyo na kila mmoja kuwa mlinzi kwa mwenzake ili
iweze kudumu na kwa muda mrefu.
Baadhi ya wananchi wa kijiji cha Likuyumandela,Mfuate na Miembeni,
wameishukuru serikali kwa jitihada za kurudisha mawasiliano ya barabara
katika maeneo hayo.
Ali Mtima mkazi wa kijiji cha Miembeni alisema,kabla ya kujengwa kwa
daraja katika mto Luegu linalounganisha kijiji hicho na
Mgombasi,walilazimika kupita kwa shida katika mto huo wenye maji mengi
hasa kipindi cha masika.
Mtima alisema,baadhi ya watu wamepoteza maisha kwa kusombwa na maji
pindi wanapohitaji kwenda kijiji jirani cha Mgombasi kufuata huduma
mbalimbali za kijamii ikiwamo huduma za afya.
Issa Amir mkazi wa Mgombasi, ameishukuru Tarura kwa kujenga barabara
zinazounganisha kata ya Mgombasi na Likuyu kwani zimerahisisha
mawasiliano na kuchochea kukua kwa uchumi wa wananchi wa maeneo hayo.
Alisema baada ya kujengwa kwa barabara hizo, sasa wanasafirisha mazao
kutoka mashambani kwenda sokoni kwa urahisi na wafanyabiashara wengi
wanafika kwa ajili ya kununua mazao wanayozalisha.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...