Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akizungumza na wananchi wa Manyoni mjini, wakati aliposimama kusikiliza kero zao, akiwa katika ziara ya kikazi mkoani Singida jana. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akizungumza na watumishi wa Halmashauri ya Manyoni na Itigi wakati akiwa katika ziara ya kikazi mkoani Singida alioianza jana. Kutoka kulia waliokaa mbele ni Katibu Mwenezi wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Singida, Ahmed Kaburu, Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake wa Chama Cha Mapinduzi (UWT) Mkoa wa Singida Jane Kessy, Katibu wa CCM Mkoa wa Singida, Lucy Boniphace, Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana UVCCM Mkoa wa Singida Dk.Denis Nyiraha na Mjumbe wa Kamati ya Siasa Mkoa wa Singida, Diana Chilolo.

Na Dotto Mwaibale, Manyoni
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa,amewagiza Wakuu wa Wilaya wahakikishe wanawasimamia Wakuu wa idara katika ukusanyaji wa mapato na utoaji wa huduma kwa wananchi kwa kupanga muda wa kwenda kuwatembelea wananchi na kusikiliza kero zinazowakabili na kuzipatia ufumbuzi.

Ameyasema hayo jana Julai 15, 2022) wakati akizungumza na watumishi wa Halmashauri ya Manyoni na Itigi akiwa katika ziara ya kikazi mkoani Singida.

“Kila mmoja ahakikishe anatekeleza majukumu yake na kutoa taarifa kwa wananchi juu ya miradi mbalimbali inayotekelezwa na Serikali katika maeneo yao," alisema.

Majaliwa alisema alichobaini viongozi was Wilaya ya Manyoni hawaendi kwa wananchi kuwasikiliza kero zao ndo maana kumakuwa na malalamiko mengi ya wananchi.

“Wakuu wa Idara hamuendi kwa wananchi kusikiliza kero zao, hamuendi kuwaeleza mwelekeo wa Serikali yetu,” alisema Mhe.Majaliwa.

Waziri Mkuu akisema Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan iko makini na haitaki mzaha katika matumizi ya fedha za umma zinazoidhinishwa kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo.

Alisema Serikali iko makini na rais alishatoa maelekezo kuwa hataki mzaha na matumizi ya fedha za umma, hakuna atakayebaki salama na hakuna mtumishi atakayeonewa.

Alisema kuna wizi mkubwa wa mapato ya Serikali kupitia mifumo ya makusanyo kwenye halmashauri nchini ikiwemo na Halmashauri ya Manyoni.

Aliagiza kuwa kila aliyepewa dhamana ya kusimamia halmashauri ajipange kusimamia makusanyo pamoja na matumizi yake.

Aidha,Waziri Mkuu amemuagiza Kamanda wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Singida Bw. Mzalendo Widege kuwahoji wakusanya mapato katika kituo cha mabasi cha Manyoni na katika mnada pamoja na Mkuu wa Idara ya TEHAMA baada kubaini ufisadi.

“Makusanyo hayasimamiwi vizuri, mfano katika kituo cha mabasi cha Manyoni Bw. Mussa Chacha ambaye si mtumishi ila amepewa kazi ya kukusanya mapato hayo kwa mwezi Juni alipeleka benki shilingi 1,786,000.”

Awali Waziri Mkuu aliweka jiwe la msingi la ujenzi wa shule ya sekondari ya wasichana ya mkoa wa Singida inayojengwa katika kata ya Solya wilayani Manyoni na kupongeza uongozi wa halmashauri hiyo kwa hatua iliyofikiwa. Shule hiyo ambayo itakapokamilika itapunguza utoro na mimba kwa wanafunzi wa kike.

Akiwa njiani kuelekea Itigi kwa ajili ya kuzungumza na watumishi wa umma, Waziri Mkuu alisimama Manyoni na kusalimia wananchi na kusikiliza kero mbalimbali zinazowakabili ikiwemo suala la machinga kutopangiwa maeneo maalumu ya kufanyia biashara zao.

Malalamiko mengine yaliyotolewa na wananchi hao ni pamoja na wajawazito kutozwa fedha pindi wanapokwenda katika hospitali ya wilaya ya Manyoni kwa ajili ya kupata huduma mbalimbali za afya licha ya Serikali kutoa huduma hizo za mama na mtoto bila ya malipo.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...