Na Bakari Madjeshi, Michuzi Tv

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema Serikali itaendelea kukopa kwa akili ili kufanya maendeleo ya nchi, amesema Serikali itaendelea kukopa mikopo hiyo yenye unafuu ili kufanya maendeleo hayo.

Dkt. Samia amesema hayo wakati akipokea ripoti ya 2021-2022 za Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) na ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG).

“Tupo vizuri labda ile asilimia 15% kwa 13% lakini tunatakiwa tusivuke hapo, mikopo ndio maendeleo, tutaendelea kukopa lakini tunakopa kwa akili,” amesema Dkt. Samia.

Hadi kufika Juni 30, 2022 deni la Serikali limeripotiwa kuwa ni kiasi cha Shilingi Trilioni 71.31 ikilinganishwa na kiasi cha Shilingi Trilioni 64.52 kilichoripotiwa mwaka wa fedha wa 2020-2021.

Kulingana na kiasi hicho, kumetajwa kuwa na ongezeko la Shilingi Trilioni 6.79 sawa na asilimia 10.5% ikilinganishwa na Shilingi Trilioni 7.79 sawa na asilimia 13.7% mwaka wa fedha uliopita.

Akisoma ripoti hiyo ya CAG mbele ya Rais Samia, Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Charles Kichere amesema katika mchanganuo huo wa deni hilo la Shilingi Trilioni 71.31, deni la Serikali linalojumuisha deni la ndani ni Shilingi Trilioni 24.04 na deni la nje ni Shilingi Trilioni 47.27 kwa mwaka wa fedha 2021-2022.

“Mwaka wa fedha 2020-2021, deni la ndani lilikuwa Shilingi Trilioni 18.93 na deni la nje lilikuwa Shilingi Trilioni 45.59 ambapo katika mwaka huo wa fedha (2020-2021) kulikuwa na jumla ya deni la Shilingi Trilioni 64.52,” amesema CAG Kichere wakati akisoma ripoti hiyo mbele ya Rais Samia.

Aidha, CAG Kichere amesema kipimo cha deni la Serikali kinachotumia pato la taifa, inaonyesha kuwa deni hilo la Serikali ni himilivu, kulingana na uwiano wa thamani ya sasa ya deni na mauzo ya nje kufikia asilimia 119.6% chini ya kikomo cha asilimia 180%.

Hata hivyo, CAG Kichere amesema uwiano wa kulipa madeni na mauzo ya nje nia asilimia 13.5% chini ya kikomo cha asilimia 15% sanjari na uwiano wa malipo ya madeni na mapato ni asilimia 14.1% chini ya kikomo cha asilimia 18%.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Viongozi mbalimbali mara baada ya kupokea Taarifa ya Ofisi ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) na Taarifa ya Taasisi ya Kupambana na Kuzuia Rushwa (TAKUKURU) kwa mwaka 2021/2022, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 29 Machi, 2023.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...